Jeshi la Polisi Mkoa wa Mwanza linafanya uchunguzi kufuatia tukio la kijana
mmoja anayesadikiwa kuwa na ugonjwa wa akili aliyewashambulia waumini
wawili na kuwajeruhi kwa panga nje ya Kanisa la Katoliki wilayani Ukerewe
wakati wa ibada,na yeye kupoteza maisha kutokana na majeraha aliyoyapata
baada ya kushambuliwa na wananchi wenye hasira kali.
Leo,Aprili 5, 2026, majira ya saa 01:30 asubuhi, katika Parokia
ya Kagunguli, Wilaya ya Ukerewe, wakati ibada ikiendelea, kijana
aliyefahamika kwa jina la Renatus Silivester, miaka 38, (maarufu kama
Pacome), mkazi wa kijiji hicho, aliingia katika kanisa hilo kupitia mlango wa
upande wa kulia akiwa amebeba mfuko na kuelekea moja kwa moja
madhabahuni, ndipo mwenyekiti wa parokia hiyo, Costantine Muumba Bituro,
mwenye umri wa miaka 65, alipomshtukia kijana huyo kutokana na mienendo
yake na kumtoa nje ya kanisa. Walipokuwa wakimhoji, kijana huyo alitoa
upanga na kuwajeruhi watu wawili.
Kutokana na kitendo hicho, kundi la waumini na wananchi waliokuwa nje ya
kanisa walimdhibiti mtuhumiwa kwa kumpiga kwa silaha za jadi na kumjeruhi
sehemu mbalimbali za mwili wake. Mtuhumiwa alikimbizwa Hospitali ya Wilaya
ya Ukerewe kwa matibabu kutokana na majeraha aliyoyapata, lakini alifariki
dunia kabla ya kufikishwa hospitalini.
Majeruhi wa tukio hilo ni Costantine Muumba Bituro, miaka 65, mwenyekiti wa
parokia, mkazi wa Kagunguli, aliyejeruhiwa kichwani na kwenye mikono yote,
na Aloyce Christopher, miaka 57, mwanakwaya, aliyejeruhiwa mkono wa
kushoto. Wote wamepelekwa Hospitali ya Kanda Bugando jijini Mwanza kwa
matibabu zaidi na hali zao zinaendelea kuimarika.
Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa kina kuhusiana na tukio hilo na
kufuatilia hali ya majeruhi waliopelekwa hospitali.
Reviewed by VISION MEDIATZBLOG
on
April 05, 2026
Rating:

No comments: