Kamanda wa Polisi Mkoa wa Manyara, Ahmed Makarani, amewataka wananchi kuendelea na shughuli zao za kila siku bila hofu, ikiwemo kusherehekea Sikukuu ya Saba Saba kwa amani, akisisitiza kuwa hadi sasa hakuna kiashiria chochote cha uvunjifu wa amani kilichorekodiwa mkoani humo.
Akizungumza kwa njia ya simu, Kamanda Makarani amesema Jeshi la Polisi limekuwa likijiandaa kikamilifu kwa zaidi ya mwezi mmoja kwa kufanya tathmini na kufuatilia viashiria vyovyote vya uhalifu vinavyoweza kuhusishwa na wito wa maandamano uliosambazwa kupitia mitandao ya kijamii, huku akibainisha kuwa hali ya usalama mkoani Manyara imeendelea kuwa shwari.
Wakati huo huo, Kamanda Makarani amesema Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa tukio la mauaji ya vijana wawili waliokuwa waendesha bodaboda, ambao waliuawa na watu wasiojulikana na kuporwa pikipiki zao.
Amesema uchunguzi unaendelea kwa lengo la kuwabaini na kuwakamata wote waliohusika na tukio hilo ili wafikishwe mbele ya vyombo vya sheria.
Reviewed by VISION MEDIATZBLOG
on
July 07, 2026
Rating:

No comments: